WANANCHI WA MKOA WA SHINYANGA KUNUFAIKA NA KAMPENI YA SAMIA LEGAL AID KWA AWAMU YA PILI..

 Na Paschazia Charles 

Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kuchangamkia fursa ya kupata huduma za msaada wa kisheria kupitia kampeni ya Samia Legal Aid Campaign itakayofanyika mkoani humo kuanzia kesho Jumatano, Mei 6,2026 mpaka May 20, 2026 katika halmashauri zote sita za mkoa huo.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa kampeni ya Samia Legal Aid mwaka 2023, imewasaidia wananchi wengi wa mkoa huo. "Kwa awamu ya kwanza, wananchi 22,261 (Elfu ishirini mbili mia mbili sitini na moja) waliwepo katika kampeni hiyo, ambapo migogoro 578 ilipokelewa, ikiwemo migogoro 317 iliyopatiwa utatuzi wa papo kwa papo na 261 iliyobaki kufanyiwa kazi," amesema Mhita.


Mhita pia amebainisha kuwa huduma hii inatolewa bure kwa siku kumi na tano kuanzia Mei 6 2026 mpaka May 20, 2026 katika Halmashauri zote  sita za mkoa huo ikiwa  ni Manispaa ya Shinyanga, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Halmashauri ya Msalala, Manispaa ya Kahama, Halmashauri ya Ushetu, na Halmashauri ya Kishapu.
"Katika Manispaa ya Shinyanga watakuwa eneo la Nguzo Nane katika viwanja vya zimamoto,Manispaa ya Kahama watakuwa kata ya Majengo, National Housing na kata ya Shunu eneo la ofisi ya mtendaji, Halmashauri ya Kishapu watakuwa Mhunze Mnadani na kata ya Ukenyenge, Community Centre,Msalala huduma itatolewa Segese uwanja wa shule na Isaka uwanja wa kosta na Ushetu katika kata ya Burungwa Centre na Nyamilangano Centre."Amesema Mhita.


Pia amesema wanufaika wakubwa wa kampeni hii ni wananchi wa kawaida ambao hupitia changamoto mbalimbali katika utafutaji wa suluhu katika mambo ya kisheria na kwamba Kampeni hii itawasaidia kupata njia sahihi za kufuata ili waweze kufikia malengo wanayoyakusudia ambapo Serikali imelenga kuwafikia zaidi wanawake, watoto, wazee, na wenye ulemavu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Uzingatiaji wa Msaada wa Kisheria, Osborn Paissi, alisema kuwa matarajio ya kampeni hiyo ni kuwafikia angalau asilimia 50 ya wananchi wenye kero za kisheria.

"Tuna matarajio ya kuwafikia asilimia 50 ya wananchi wa Shinyanga kwa huduma za utoaji elimu ya kisheria, uandaaji wa masuala ya kisheria, kutoa uwakilishi wa mahakamani katika mabaraza, usajili wa vyeti vya kuzaliwa na vifo sambamba na utoaji wa hati ya umiliki wa ardhi kwa muda mfupi," alisema Paissi.

Paissi aliongeza kuwa katika awamu ya kwanza ya mwaka 2023, asilimia 33 ya migogoro yote ilikuwa ni migogoro ya ardhi.
"Katika kipindi hiki, tumejipanga kutoa elimu ya umiliki wa ardhi na mipaka ya ardhi, jambo litakalosaidia kupunguza idadi ya migogoro ya ardhi," alisema Paissi.


Kampeni hiyo itafanyika kwa siku 15 kuanzia Mei 6 hadi Mei 20, 2026, ikihusisha timu ya wataalamu wa masuala ya kisheria. Huduma zinazotolewa ni pamoja na ushauri wa kisheria, elimu kuhusu sheria, pamoja na uandaaji wa nyaraka za kisheria.






Download/Pakua/Install App ya APA HABARI Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia apahabarikadama@yahoo.com
Previous Post Next Post